Viongozi wa Serikali za Mitaa Kilimanjaro Watakiwa Kuzingatia Maadili, Misingi ya Utawala Bora

MOSHI-KILIMANJARO.

Serikali mkoa wa Kilimanjaro, imewataka viongozi na watendaji wa mamlaka za serikali za mitaa, kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na maadili ili kulinda misingi ya utawala bora.

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, aliyasema hayo Februari 3,2025, wakati akifungua mafunzo kwa wajumbe wa kamati ya usalama ya Mkoa, wajumbe wa kamati ya usalama ya wilaya ya Moshi, watendaji wa kata na wakuu wa idara wa wilaya hiyo, wakati wa mafunzo kuhusu elimu ya Uraia na Utawala Bora  yaliyofanyika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa huo.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa, Katibu Tawala wa mkoa huo Kiseo Nzowa, aliwataka viongozi hao kuhakikisha kwamba pindi wanapotekeleza majukumu yao ya kazi, wazingatie haki za binadamu, utawala bora, maadili na miiko ya uongozi.

“Napenda kuipongeza Wizara ya Katiba na Sheria kwa kubuni na kuendesha mafunzo haya muhimu ya masuala ya Uraia na Utawala Bora kwa Kamati za Usalama na Watendaji wa halmashauri .”alisema Kiseo.

Alisema mkoa wa Kilimanjaro, unakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa haki za binadamu na uzingatiwaji wa misingi ya utawala bora huku akizitaja changamoto hizo kuwa ni pamoja na uelewa mdogo wa misingi ya haki za binadamu miongoni mwa jamii.

“Mafunzo haya yanafanyika kwa wakati muafaka kwa kuwa katika mkoa  wetu wa Kilimanjaro zipo changamoto kadhaa katika utekelezaji wa haki za binadamu na uzingatiwaji wa misingi ya utawala bora, baadhi ya changamoto hizo ni pamoja na uelewa mdogo wa misingi ya haki za binadamu miongoni mwa jamii, mila na destuli kandamizi, vitendo vya ukatili wa kijinsia na vitendo vya ubakaji,”alisema.

Awali akizungumza Mkurugenzi wa Idara Katiba na Ufuatiliaji Haki kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Jane Lyimo, alisema Wizara ya Katiba na Sheria imeendelea  kuwa kinara kwa kutekeleza kwa vitendo na kuiishi falsafa ya 4Rs ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa vitendo ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

“Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, kwa jitihada za kuendelea kuwapambania wananchi wake kupitia falsafa yake ya 4Rs na sisi kama Wizara ya Katiba na Sheria ni moja ya vinara wa utekelezaji wa falsafa hizi,”alisema Lyimo.

Akiwasilisha mada ya Ulinzi na Usalama wa Nchi kwa washiriki wa mafunzo hayo Mrakibu Msaidizi wa Polisi, Wakili wa Serikali Nicholaus Mhagama, aliwasihi watendaji kata, kuacha kung’ang’ania kutatua migogoro  ambayo hawajaisomea, huku akitolea mfano wa migogoro ya ndoa ambayo walikuwa wakiitatua kwa kutumia uzoefu badala ya elimu maalum.Kwa upande wake Afisa Uchunguzi Mkuu  kutoka Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) Juliana Raurent, alisema ukiukwaji wa haki za binadamu unachangia umasikini mkubwa katika jamii.

“Suala la umasikini ni changamoto kubwa amabayo inafanya haki za binadamu ziweze kuvunjwa pasipo sisi wenyewe kuzitambua , kwa umasikini huo anajikuta anadhalilika utu wake, lakini pia mila na desturi tulizonazo ni changamoto kubwa kwa jamii yetu.”








Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.