Wagonjwa wanaotibiwa hospitali ya Kibong'oto waishukuru Serikali kwa kuchukua jukumu la kulipia gharama za matibabu ya Kifua Kikuu

MKOMAZI-SAME.

Baadhi ya wagonjwa waliotibiwa, Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH) iliyoko Wilaya ya Siha, mkoani Kilimanjaro, wameipongeza Serikali kwa kuchukua jukumu la kulipia gharama za matibabu ya Kifua Kikuu hospitalini hapo.

Wagonjwa hao walitoa shukrani hizo jana, wakati wa ziara ya siku moja katika Hifadhi ya Taifa Mkomazi, iliyoko Wilaya ya Same mkoani humo, iliyoandaliwa na uongozi wa hospitali hiyo, ambapo walisema uamuzi huo wa Serikali kuwagharamia matibabu yao, umewawezesha kuokoa maisha yao kutokana na ukweli kuwa gharama za matibabu ya ugonjwa huo ni kubwa sana.

Akizungumza mmoja wa wagonjwa waliotibiwa Kifua Kikuu Sugu (TB), hospitalini hapo na kupona kabisa Ally Seif Salim alisema “Mbali na huduma za matibabu kuwa ni za juu sana, pia Serikali inagharamia vipimo kabla ya kuanza matibabu, chakula na mavazi wakati wa kipindi chote cha matibabu ambacho ni kirefu sana”,alisema.

“Wakati nilipoletwa katika hospitali ya Kibong’oto hali yangu ilikuwa mbaya sana, kiasi cha kupoteza matumaini yangu ya kuishi, lakini kwa sasa nimepona kabisa.”alisema.

Mnufaika mwingine Hansibari Ally Mvita kutoka mkoa wa Lindi, alisema baada ya kusumbuka na TB kwa muda mrefu, hatimaye aliletwa hospitali ya Kibong’oto na kuanza kupatiwa matibabu ambayo yalimwezesha kupona kabisa.

“Nilikuwa nikisumbuliwa na maumivu ya kifua kwa miaka mingi sana na nilihangaika kwa muda mrefu haswa kwenye tiba za asili; hali ilipofikia kuwa mbaya, baada ya kuanza kutapika damu nilipekwa hospitali ya Nachingwea na kugundulika nilikuwa na ugonjwa wa Kifua Kikuu Sugu (TB),”, alisema Mvita.

Alisema baada ya kugundulika kuwa na TB Sugu, alipatiwa rufaa ya kuletwa hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto na kuanzishiwa matibabu chini ya ufadhili wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia na sasa nimepona.

Kwa upande wake mnufaika mwingine Husna Sabato kutoka Musoma mkoa wa Mara, ambaye alibainika kuwa na TB  Sugu, alimshukuru  Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha kugharamia matibabu yake na kuweza kupona kabisa ugonjwa huo, bila kutumia gharama zozote.

“Ninaushukuru sana uongozi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH), chini ya Mkurugenzi wake Dk. Leoinard Subi, kwa namna inavyojitahidi kwa kila hali kuhakikisha Kifua Kikuu Sugu kinatokomezwa kwa watu wazima na watoto.”alisema.

Akizungumiza safari ya kutembeleea hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Mvita alisema amefarijika sana kuwaona wanyama aina ya Faru weusi na Mbwa Mwitu,  wanyama ambao hakuwahi kuwaona na kwamba ziara ya mbugani imemuondolea mawazo ya kukaa kwenye tiba kwa muda mrefu jambo ambalo alisema pia lilimfanya kuwa mbali na familia yake  kwa muda mrefu na kujihisi kwamba ametengwa.

Akizungumzia safari hiyo, Afisa Ustawi wa Jamii Hospitali Maalum ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto Wazoeli Mshana, alisema uongozi wa (KIDH), ulianzisha programu hiyo tangu mwaka 2022 ya kuwapeleka mbuga za wanyama wagonjwa wa Kifua kikuu waliotibiwa na kupona ili kuwafariji kutokana na kukaa kwenye matibabu kwa muda mrefu.

“Wagonjwa hawa huwa wengi wao wanatoka nyumbani kwao kuja kwa matibabu na hukaa kwa muda mrefu, kati ya miezi sita hadi tisa bila ya kutoka hospitalini, hivyo tukaona baada ya kupona ni vyema wakapata fursa ya kujifariji ndipo tukaja na wazo la kuwapeleka watembelee hifadhi za Taifa”, alisema.

Akizungumzia uamuzi wa Serikali kugharamia matibabu ya kifua kikuu, Mshana alisema hatua hiyo ni mkombozi mkubwa kwa wagonjwa ambao wangelazimika kutumia gharama kubwa sana za matibabu ya Kifua Kikuu haswa kwa wale ambao wamefikia hatua ya kuwa na ugonjwa wa Kifua Kikuu Sugu TB.

“Gharama za kumtibu mgonjwa wa Kifua Kikuu cha kawaida ni kati ya SH milioni 12 na milioni 15, wakati Kifua Kikuu Sugu (TB), matibabu yake ni kati ya Sh milioni 15 hadi milioni 40 kwa mtu mmoja; na hii inatokana na mgonjwa kuhitaji kama kukaa hospitalini hapa kati ya miezi sita hadi tisa ili apone kabisa”, alisema.

Aidha Mshana aliipongeza Taasisi ya LHL International, kwa ksuhirikiana na Serikali kulipia baadhi ya gharama za matibabu na mahitaji mengine kwa ajili ya wagonjwa wa Kifua Kikuu wanaopata tiba hospitalini hapo.

Kwa upande wake Dk. Lilian Mahemba kutoka kitengo cha Kifua Kikuu Sugu, alisema dhana ya kuwapeleka waliopona kutembelea hifadhi za Taifa kuna wawezesha kubadili mazingira na pia kuwaongezea furaha wanazopata baada ya kupona ugonjwa ambao umewasumbua kwa muda mrefu.

Aidha alitoa ushauri kwa wananchi wanapojisikia hali tofauti kwenda mara moja kwa wataalam wa afya ili wakigundulika ya kuwa wanamaradhi ya Kifua Kikuu wapate huduma za mapema ambazo zitawasaidia kupona kabisa.

Naye Anjela Kimaro kutoka kitengo cha Fiziotherapia ambacho kinahusika na mazoezi ya upumuaji na viungo kwa wagonjwa wa Kifua Kikuu, alisema mazoezi hayo huwasaidia wagonjwa kuongeza uwezo wa kupumua jambo ambalo linawapa unafuu na hivyo kupata nafasi ya kupata tiba na hatimae kupona kabisa.

“Tunawashirikisha kufanya mazoezi ambayo yatahusisha upumuaji ambayo yatamsaidia mgonjwa wa Kifua Kikuu, kuongeza uwezo wa mapafu kuweka hewa zaidi na kutanua mapafu zaidi ili hewa iweze kukidhi mahitaji ya mwilini”, alisema.














Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.