PBWB yapongezwa kwa juhudi za kutunza vyanzo vya maji na maliasili

SAME-KILIMANJARO.

Waziri wa Maliasili na Utalii Balozi  Dk. Pindi Chana, ameipingeza Bodi ya Maji Bonde la Pangani (PBWB),kwa juhudi zao za kutunza vyanzo vya maji na maliasili zilizopo nchini.

Dk. Chana  alitoa pongezi hizo hivi karibuni, akiwa Wilayani Same mkoani Kilimanjaro, wakati akifungua Msimu wa Pili  wa  Tamasha la Utalii  Same, ambapo alisema ufanisi wa Bodi hiyo, umewezesha rasilimali za maji kutunzwa kwa njia endelevu na hivyo kuleta manufaa kwa jamii na mazingira kwa ujumla.

Waziri Chana, alitaja juhudi za viongozi hao katika kukuza sekta ya utalii kama mfano mzuri wa ushirikiano na uongozi bora, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea na juhudi hizo, ili kudumisha ustawi wa mazingira na kuhakikisha upatikanaji wa maji safi na salama kwa vizazi vijavyo na kwa maisha ya wanyama.

Aidha Waziri Chana, aliwataka wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro, kuhakikisha wanaunga mkono jitihada zinazofanywa na Bodi ya Maji Bonde la Pangani kwa kuvitunza vyanzo vya maji na kusema kuwa Serikali haitamuacha salama mtu yeyote atakayehusika na kuharibu vyanzo vya maji.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Pangani, Afisa Maendeleo ya Jamii Bodi ya Maji Bonde la Pangani (PBWB), Patrice Otieno, alisema kuwa kutokana na elimu ambayo imekuwa ikitolewa na Bodi, baadhi ya wananchi wameanza kupata uelewa na kuanza kuchukua hatua muhimu katika kuhifadhi vyanzo vya maji.

“Tunafahamu matumizi ya maji ni mengi sana hususani kwa wakulima ambao hutumia maji mengi kwa ajili ya kilimo na umwagiliaji,  lakini tumekuwa tuhakikisha maji haya pia yanatiririka kwenda kwenye mbuga ili  wanyama  na mimea iweze kupata maji pia.”alisema Otieno.

Aidha Otieno, alisema Bodi ya Maji Bonde la Pangani, itaendelea kuhakikisha kwamba maeneo yote yenye vyanzo vya maji kuanzia kwenye milima, mabonde, mito, maziwa na chemichem, zinaendelea kuwa na maji kwa kuyahifadhi, ikiwa ni sambamba na kupanda miti kwa wingi pamoja na kuweka mabango yyenye makatazo ya kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya mita 60.








Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.