Asilimia 43 ya watu wanaoishi na maambukizi ya Kifua Kikuu wanakutana na changamoto za afya ya akili


SIHA-KILIMANJARO

Tafiti zinaonyesha kuwa asilimia 43 ya watu walio na magonjwa ya maambukizi ukiwemo ule wa Kifua Kikuu, wanapata changamoto ya afya ya akili.

Changamoto hiyo inasababishwa na sonona ambayo inasababishwa na mawazo mengi wanayokuwa nayo wagonjwa hao kutokana na kuugua kwa muda mrefu.

Hayo yameelezwa na Daktari Bingwa wa Magonwja ya Akili kutoka hospitali ya Taifa Muhimbili Saidi Kuganda wakati wa semina ya siku nne, kwa ajili ya madaktari na wauguzi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH) iliyofanyika Siha, mkoani Kilimanjaro.

“Watu wengi wakipata maradhi ambukizi haswa yale yanayochukua muda mrefu, hujikuta wakiwa na mawazo mengi kutokana na kuwa na maradhi hayo na kuwafanya waache shughuli zao, hili huwasababishia kuwa na msongo wa mawazo na hatimae kujikuta wakiingia kwenye changamoto ya afya ya akili”, alisema.

Akizungumzia tahadhari ambayo watu wanahitaji kuchukua ili kuepuka changamoto ya maradhi ambayo husababisha afya ya akili, Dk. Kuganda alisema hawanabudi kuepuka tabia ya kutumia dawa za kulevya.

“Matumizi ya dawa za kulevya haswa yale ya kutumia sindano ambazo hujichoma wahusika husababisha kuchangia maambukizi ya maradhi ambayo hatimae hupelekea mtu kuwa na changamoto ya afya ya akili hapo baadaye”, alisema na kuongeza, watu hawana budi kujiepuesha na mitindo ya maisha kama vile matumizi ya dawa za kulevya ambayo yanaweza kuharibu maisha yao ya baadaye.” Dk. Kuganda.

Akifugua semina hiyo, Mkurugenzi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH) Dk. Leonard Subi amesema semina hiyo inalenga kuwaelimisha watoa huduma za afya hospitalini hapo kuhusu jinsi ya kutambua na kuwuhudumia wagonwja wenye chanagmoto ya akili haswa wale wanaougua muda mrefu.

“Wawezeshaji katika semina hii wametoka MUHAS na Chuo kikuu cha Kikatoliki Mwenge (MWECAU) ambapo watawajengea wataalam wetu hapa KIDH uwezo na namna bora ya kuwahudumia wagonjwa wetu, ambao huwa tunakaa nao kwa muda mrefu”, alisema Dk. Subi.

Aliongeza, “Kama mnavyofahamu wagonjwa katika hospitali yetu ya Kibong’oto wanatoka maeneo mbalimbali na matibabu yao ni ya muda mrefu, hivyo ni vyema wataalam wetu wakapata elimu ya ziada ya jinsi ya kuwahudumia haswa ikitiliwa maanani wanakaa na wagonjwa hao kwa muda mrefu sana”.

Aidha Dk. Subi aliwashukuru wafadhili kutoka LHL International kutoka nchini Norway, ambao wamefadhili semina hiyo sambamba na kufadhili matibabu ya wagonjwa wanaopata huduma zao hospitalini hapo kwa mdua mrefu.

“Wafadhili hawa pamoja na Serikali wamekuwa wakitoa msaada mkubwa katika kutoa huduma za chakula, nguo, dawa pamoja elimu ambayo KIDH hutoa maeneo mbalimbali hapa nchini kuhusu jinsi ya kujikinga na maambukizi ya kifua kikuu”, alisema Dk. Subi.

Kwa upande wa mtaalam wa afya ya akili (Mwanasaikolojia) kutoka Chuo cha Kikatoliki Mwenge Godfrey Mbowe, amesema warsha hiyo, imelenga kuwawezesha watoa huduma za afya, madaktari na wauguzi kujua vionjo vya kiseikolojia vitakavyo wasaidia jinsi ya kushughulika na wagonjwa.

Naye mtaalam wa huduma za kisaikolojia (Psychological Care) kutoka hospitali maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto Leocadia Tito Mtweve amesema, mafunzo hayo yamewahusisha wauguzi wanatoa huduma kwa wagonjwa wa TB Sugu (MDR).

“Tumeona ni vizuri watumishi hawa ambao ni madaktari na wauguzi wanaotoa huduma kwa wagonjwa Kifua Kikuu wapate elimu inayohusiana na afya ya akili kwani wanakaa na wagonjwa hawa kwa mrefu hivyo wanapitia changamoto mbalimbali,” alisema Mtweve.

Afisa Ustawi wa Jamii KIDH Wazoel Yohana Mshana, Amesema mafunzo ya afya ya akili, kwetu sisi  yatakuwa na tija, kwani kwa kipindi kirefu  tumekuwa tukiwahudumia wagonjwa wa TB Sugu, wanaotoka katika mikoa tofauti hapa nchini  ambao wanakuja na tamaduni zao tofauti.

“Kupitia mafunzo haya ambayo yameratibiwa na taasisi ya LHL International, kwetu sisi wafanyakazi yatatusaidia namna ya kupambana na magonjwa haya ya afya ya akili kwani yamekuwa yakitupa wakati mgumu katika kuhudumia wagonwja wenye changamoto hizo”, alisema.Mkurugenzi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH) Dk. Leonard Subi, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Warsha ya siku Nne ya kuwajengea uwezo Madaktari na Wauguzi wanaowahudumia wagonjwa wa Kifua Kikuu ambao wana kaa kwa muda mrefu hospitalini.

Dk. Leonard Subi (kushoto) Mkurugenzi wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto akisalimiana na Daktari Bingwa wa Magonwja ya Akili kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili Saidi Kuganda.

Daktari Bingwa wa Magonwja ya Akili kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili Saidi Kuganda

Mtaalam wa Afya ya Akili (Mwanasaikolojia) kutoka Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mwenge Godfrey Mbowe (MWECAU).

Mtaalam wa Huduma za Kisaikolojia (Psychological Care) kutoka Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto Leocadia Tito Mtweve.
Mhadhiri Chuo cha Afya Mhimbili ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Afya na Magonjwa ya akili Hospitali ya Taifa (MUHAS) Saidi Kuganda (kushoto) akiwa na Mtaalam wa afya ya akili (Mwanasaikolojia) kutoka Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mwenge (MWECAU) Godfrey Mbowe, walioshiriki kwa ajili ya kutoa semina inayohusiana na afya ya akili kwa madaktari na wauguzi  wanaokaa  na wagonjwa kwa muda mrefu. 

Katibu wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto (KIDH) Rose Shawa.




Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.