Wizara ya Afya, Tamisemi kuanza kushirikiana kutoa elimu ya afya mashuleni

Mwanafunzi Rosemary Shirima, akimshukuru Naibu Waziri wa Afya Dk. Godwin Mollel, kwa namna alivyomsaidia katika matibabu yake na akaweza kufanyiwa upasuaji mkubwa wa tumbo hospitali ya Taifa Muhimbili.

SAME-KILIMANJARO.

Naibu Waziri wa Afya Dkt Godwin Mollel amesema Wizara ya afya inaangalia uwezekano wa kushirikiana na Wizara ya Tamisemi ili kuanza mchakato wa kutoa elimu ya afya mashuleni.

Dkt Mollel aliyasema hayo hivi karibuni, wakati akiwa mgeni rasmi katika mahafali ya tatu ya kidato cha nne shule ya sekondari ya New Dawn, iliyoko  kata ya Njoro halmashauri ya wilaya ya Same, Mkoa wa Kilimanjaro.

Amesema “Kwenye shule zetu, ikiwemo shule ya New Dawn, kuna wanafunzi wanaotoka kwenye mazingira magumu, mara nyingi, wengi wanakuwa wameathirika na mambo mengi yanayohusiana na maswala ya kifamilia tangu utotoni”, amesema Dk. Mollel.

Amesema kutokana na hali hiyo baadhi ya wanafunzi wenye changamoto za namna hiyo huwa wanafanya maamuzi ambayo yanaonyesha wazi ya kuwa wameathirika kwa njia moja au nyingine na hivyo kupeleka tafsri ya moja kwa moja ya kuwa wanachangamoto za kiafya.

“Sisi kama Wizara ya afya tunataka tuone namna ya kushirikiana na wenzetu wa TAMISEMI, ili kushughulikia maswala yanayohusiana na afya ya akili, kwenye shule ambazo zinadahili wanafunzi kutoka sehemu mablimbali na wengi wao wakiwa ni wale wanaoishi katika mazingira magumu”, amesema.

Ameongeza “Kama Rais Samia Suluhu Hassan, alipozindua mpango wa lishe mashuleni, pia kwenye eneo la afya kuna haja kuwa na mpango maalum unahusiana na maswala ya afya ya akili kwa ksuhirikiana na taasisi za kiafya za wilaya na mikoa”, amesema na kuongeza, afya nzuri ya akili ni msingi bora utakaowawezesha wanafunzi kufanya vyema kwenye masomo yao.

Vilevile Dk. Mollel,  akatoa rai kwa maofisa afya wa ngazi zote kupita mashuleni kufanya utafiti, ambao matokeo yake yatakuwa msingi wa kuanza kutoa elimu inayohusiana na afya ya akili mashuleni.

Aidha ameushukuru uongozi wa shule ya New Dawn kwa kuanzisha shule hiyo, ambayo pamoja na mambo mengine inatoa elimu ya sekondari kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu na yatima hadi kidato cha nne bila kuchangia gharama zozote.

“Uamuzi wa kuanzisha shule hii umekuwa faraja si kwa wanafunzi tu bali na hata sisi ambao tulikuwa tunachangia masomo ya baadhi ya wanafunzi wanaoishi katika mazingira magumu”, amesema.

“Mimi mwenyewe nilikuwa nachangia kati shilingi milioni 9 na milioni 10 kwa mwaka kwa ajili ya kuchangia ghrama za masomo kwa wanafunzi wanaoishi katika mazingira magumu, wanaotoka katika Jimbo langu la Siha, lakini jukumu hili kwa sasa linashughulikiwa na shule hii ya New Dawn”, amesema na kuongeza, kazi mnayofanya haina budi kuungwa mkono.

Awali akizungumza Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la New Dawn Community  Dkt.  Stephano Mshomi, amesema uongozi wa shule umekuwa ukishirikina vizuri na idara za afya kuanzia zahanati iliyopo kijiji cha Ishinde kwa kuwapa matibabu wanafunzi wenye changamoto za kiafya.

“Tumekuwa tukipata ushirikiano mkubwa kuanzia kwa wataalam wa afya walioko kwenye zahanati ya kijiji, pamoja na hospitali ya wilaya ya Same, hospitali za rufaa ya Kanda ya Kaskazini KCMC, na hospitali ya Taifa ya Muhimbili,”amesema  Dk. Mshomi.

“Wanafunzi watatu walifanyiwa upasuaji kati yao wawili walifanyiwa upasuaji wa kidole tumbo na mmoja alifanyiwa upasuaji mkubwa wa tumbo mara tatu hospitali ya Muhimbili.

Wakitoa  ushuhuda wao wa namna ambavyo uongozi wa shule pamoja walivyo wasaidia kuokoa maisha yao Rosemary Shirima, na Nusra Mohamed, hawakutarajia kama wangekuwa wako hai hadi leo hii.

“Nilikuwa na hali mbaya sana, mimi mwenyewe sikutegemea kama ningekuwa hai hadi leo na kuweza kuhitimu elimu yangu ya kidato cha nne,”amesema Rosemary.







 

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.