Tarura yaombwa kuharakisha ujenzi wa barabara ya Ndea


MWANGA-KILIMANJARO

Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Mwanahamisi Munkunda, ameitaka Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) Wilayani humo, kuharakisha ujenzi wa barabara ya Karamba ndea, inayoelekea kwenye lango la hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, jambo ambalo litakuza utalii na mapato ya halmashauri kwa ujumla.

Munkunda, aliyasema hayo Desemba 27,2024, wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa Tamasha la michezo lijulikanalo kama (Mwanga Marathon and Festival 2024), lililofanyika katika viwanja vya CM Msuya.

Alisema kufunguliwa kwa lango hilo, litakwenda kukuza utalii na kuongeza mapato ya mtu mmoja mmoja, halmashauri na taifa kwa ujumla.

Aidha alisema Wilaya hiyo pia ina lengo la kuanzisha forodha ndogo kupitia lango hilo, ili kusaidia watalii wanaotoka hifadhi ya Taifa Tsavo nchini Kenya ili waweze, kupata huduma za kiforodha ndani ya lango hilo.

“Ninamshukuru na kumpongeza sana Mkurugenzi wa Kisangara Tours Frida Mberesero, kwa kazi kubwa ambayo ameifanya ya kuviibua na kuvionesha vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo wilaya hapa, ambavyo tutavitumia kama sehemu ya kuchochea utalii ndani yetu,”alisema DC Mnkunda.

Alisema kama Wilaya pia wamejipanga, kuhakikisha kwamba maeneo yote ya utalii wanakwenda kuyalinda ili kuchochea uchumi pamoja na kuwakaribisha wawelezaji wa ndani, kuja kuwekeza kwenye sekta ya utalii.

Kwa upande wake Katibu Tawala mkoa mkoa wa Kilimanjaro Kiseo Nzowa, aliutaka uongozi wa wilaya hiyo kuhakikisha kwamba wanavitangaza vivutio vya utalii vilivyopo ili kuvutia wawekezaji wengi kuja kuwekeza ndani ya wilaya hiyo.

Naye Mbunge wa Jimbo la Mwanga Joseph Tadayo, alisema mkakati wa serikali ni kwenda kulifungua lango la Karamba Ndea  ili kukuza sekta ya Utalii,  na kuongeza mapato ya halmashauri.

































Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.