Nurdin Babu Mgeni Rasmi Mbio za Mwanga Festival and Marathon

MWANGA-KILIMANJARO

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika Mbio za Mwanga Festival and Marathon-2024 zitakazofanyika desemba 27, mwaka huu Wilayani humo.

Akizungumza na waandishi wa habari desemba 26,2024, kuhusu hali ya maandalizi ya mbio hizo, Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Mwanahamisi Mnkunda, amesema Mkuu wa Mkoa amekubali mwaliko wa kuwa Mgeni Rasmi wa mbio hizo zinazolenga kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo wilayani Mwanga.

DC Mnkunda, amesema Babu ndiye atakayeanzisha mbio hizo ambazo zitaanzia uwanja wa CD Msuya, huku akiwataka  wananchi wa Mwanga, kuzipokea mbio hizo kama dirisha la kiuchumi na kujiandaa kuendena na ongezeko la mahitaji ya kijamii.

Amesema mbio za Mwanga Festival and Marathon, zinatarajia kuwaleta pamoja watu zaidi ya 1,000, ambao  watahitaji chakula, malazi, mavazi, usafiri, na aina nyinginezo za burudani, huku akitoa shime kuchangamkia fursa hiyo.

“Mwanga Festival and Marathon, tunatarajia kuwaleta watu zaidi ya 1,000, ambao  watahitaji chakula, malazi, mavazi, usafiri, na aina nyinginezo za burudani, shime tuitumie fursa hii kujipanga vilivyo, Wilaya ya Mwanga  ina mengi ya kutoa; tuchangamkie fursa hiyo,” amesema DC Mnkunda.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mwanga Festival and Marathon Frida Mberesero, amesema jumla ya wanariadha 500 kutoka Wilayani humo, wanatarajia kushiriki mbio hizo, zijulikanazo kama za Mwanga Festival and Marathon Season One 2024 zitakazofanyika Desemba 27, mwaka huu.

Amesema maandalizi ya mbio hizo, yamefikia asilimia 100 ambapo wanaridha 500 watashiriki mbio hizo, zikiwa na lengo la kuvitangaza vivutio vya utalii vilivyopo wilayani humo.

“Huu ni msimu wetu wa kwanza wa mbio hizi za Mwanga Festival and Marathon, tunashukuru wananchi wa Mwanga wamehamasika kwa wingi kushiriki mbio hizi,”amesemaMberesero.

Amesema mbio hizo zitakuwa za kilometa 5 na Km 10 ambazo zitaanzia uwanja wa CD Msuya majira ya saa kumi na mbili kamili alfajiri, ambapo pia zitashirikisha vijana, watoto na wazee, huku Kauli Mbiu ya mbio hizo ni “Kuvumbua na Kuboresha Vivutio vya Asili Vilivyopo Wilaya ya Mwanga.”

Akizungumza  mmoja wa washiriki wa mbio hizo,  Rajabu Mshana, ambaye amejiandikisha kukimbia mbio za Km 10 amesema ameshawishika  kukimbia mbio hizo, baada ya kuvutiwa na nia ya waandaaji hao, waliokuja na wazo la kuvitangaza vivutio vya utalii vilivyopo wilayani humo.














Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.