Bima ya Afya kwa wote kuwapunguzia wananchi gharama za matibabu

MOSHI-KILIMANJARO

Kuanza kutumika kwa Bima ya Afya kwa Wote, kutasaidia kupunguza gharama za matibabu ya Kibingwa yakiwemo magonjwa ya moyo na hivyo kuwaondolea wananchi mzigo mkubwa wa kulipia gharama za matibabu.

Hayo yamesemwa Desemba 4,2024 na Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, wakati wa ufunguzi wa Kambi ya Madaktari Bingwa na Bingwa Bobezi wa Dk. Samia Suluhu Hassan Kanda ya Kaskazini, walioweka kambi ya siku Tano kuanzia Desemba 2 hadi Sita katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa Mawenzi.

Akizungumza na wagonjwa waliofika kutibiwa hospitalini hapo, Babu amesema gharama za matibabu ya Kibingwa ni kubwa na Serikali imekuwa na jukumu kubwa la kulipia gharama hizo za matibabu kwa watu wasiokuwa na uwezo wa kulipia, hivyo kuanza kutumika kwa Bima ya Afya kwa wote, kutasaidia Wananchi kupata huduma popote walipo hata kama hawatakuwa na fedha mfukoni  katika kipindi ambacho wataugua.

“Niwaombe sana Bima ya Afya kwa Wote, itakapoanza kutumika, mjiunge kwani itasaidia kupata matibabu mahali popote pale mlipo na itasaidia kufuatilia matibabu ya mgonjwa kutoka hospitali yoyote nchini.”amesema Babu.

Aidha mkuu huyo wa mkoa, amewashukuru Madaktari Bingwa kutoka Hospitali ya Rufaa ya Bombo-Tanga, Maunt Meru Jijini Arusha, Manyara, Hospitali ya Rufaa ya mkoa Mawenzi, KCMC, Benjamini Mkapa na Hospitali ya Rufani ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi ya Kibong'oto (KIDH), kwa kukubali kuja kutoa huduma katika mkoa huo.

Pia amesema kuwa, katika kuboresha huduma za afya nchini, mkoa wa Kilimanjaro, umekwisha kupokea  kiasi cha Sh bilioni 129, fedha ambazo zimetumika kujenga hospitali mpya  wilaya ya Same, Mwanga, Moshi Vijijini na Manispaa ya Moshi, huku Wilaya ya Hai, ikipokea fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba na  ukarabati wa miundombinu.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa mkoa wa Kilimanjaro KiseoYusufu Nzowa, amesema mwanadamu anapopungukiwa na rasilimali ya afya utu wake, thamani yake, ubora wake unapungua kwa kiasi kikubwa na katika kulitambua hilo, Serikali imeamua kufanya maboresho makubwa kwenye sekta ya afya kwa lengo la kuwawezesha wananchi wake waweze kuwa na afya bora wakati wote. 

“Natamani wananchi wafike kwa wingi mahali ambapo huduma hizi zinatolewa na wataalam wa afya, kwani Rais Samia Suluhu Hassan,  anawajali wananchi wake, ndiyo maana amesogeza huduma hii karibu na maeneo yenu baada ya kuona changamoto wanazokutana nazo,”amesema Nzowa.

Awali akizungumza Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi Dk. Edina-Joy- Munisi, amesema jumla ya wagonjwa 1,328 wameweza kuwaona na kati yao wagonjwa 22 wamefanyiwa upasuaji.

Baadhi ya wagonjwa waliofika kutibiwa katika hospitali hiyo, Mary Andrea Mbowe, Aisha Amiri Kidusho, wameshukuru kwa huduma za matibabu walizozipata kutoka kwa timu ya madaktari bingwa na bingwa bobezi wanazozitoa na kusema kuwa kwa kiwango kikubwa wamesaidia kuokoa maisha yao na ya watoto wao.

















Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.