Wafanyakazi TPC wachangishana kununua gari la wagonjwa


MOSHI-KILIMANJARO.

Wafanyakazi wa Kiwanda cha  sukari cha TPC kilichopo Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro, wametumia sehemu ya mishahara yao  kufanikisha kununua gari la wagonjwa.

Mwenyekiti wa Bodi ya FT-Kilimanjaro Jaffari Ally, ameyasema hayo wakati wa kukabidhi gari hilo aina ya Toyota Land Cruseir lenye thamani ya Sh milioni 219, ambalo limekabidhiwa katika hospital ya TPC iliyopo chini ya usimamizi wa kiwanda hicho.

Alisema gari hilo litakuwa likitoa huduma za afya kwa akina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano.

Amesema lengo la kuanzishwa kwa mradi wa Mama Bus ni kutokana na  kuwepo kwa changamoto ya usafiri kwa makundi hayo, waliokuwa wakilazimika kutembea umbali wa kilometa 20 kutafuta huduma za matibabu.

Hatua hiyo inatajwa kuwepo na vifo vingi vya mama wajawazito na watoto iliyotokana na kutokuwepo kwa huduma za afya karibu.

“Mradi wa Mama Bus tulianza na vijijiji vinne ambavyo ni Kiyungi, Kikavu, Mbuyuni na Utamaduni ndani ya Arusha Chini na tumeongeza na kufikia vijiji tisa ambavyo ni Uhuru, Langaseni, Mikocheni, Chemchem na Muungano ,ambapo Mama Bus hutembea kila siku kijiji kimoja na kutoa huduma hizo.”amesema.

Ally aliongeza kuwa mradi huo wa Mama Bus utawanufaisha wananchi wapatao 95,000 katika kata za Arusha Chini iliyopo Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro na Kata ya Msitu wa tembo iliyopo wilaya ya Simanjiiro mkoani Manyara.

Alisema kuwa kupatikana kwa gari hilo kumechagizwa na mishahara ya wafanyakazi wa kiwanda hicho ambao  walikuwa wanakatwa mishahara yao kidogo kidogo na kufanikisha ununuzi wa gari hilo.

“Kundi la akina mama wajawazito na watoto ni makundi ambayo yanaambukizwa magonjwa ya mlipuko kwa haraka hivyo FT-Kilimanjaro imefanya jitihada za kuokoa maisha ya makundi haya kwa kuwasogezea karibu huduma za afya.”amesema Ally.

Kwa upande wake msimamizi wa miradi ya FT-Kilimanjaro  Lazaro Urio, amesema awali walikuwa wakitoa huduma hiyo kwa kutumia gari aina ya Noah, ambayo kwa sasa imechakaa kutokana na ubovu wa barabara hali ambayo ilikuwa inahatarisha maisha ya mama wajawazito na watoto.

Amesema  kuanzishwa kwa mradi huo kumesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa maeneo ya Moshi Vijijini mkoani Kilimanjaro na  upande wa Simanjiro mkoani Manyara.

“Tumekuwa tukitoa huduma za afya kwa kutumia gari aina ya Noah kwa zaidi ya miaka 10, kwa kipindi cha masika gari hii ilikuwa haiwezi kwenda kutokana na uchakavu wa barabara, tunawashukuru wadau wa maendeleo  waliojitokeza kununua gari hili wakiwemo kampuni ya mafuta PUMA, Toyota, TPC na FEMI.”amesema.





Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.