TAPSEA Kilimanjaro yatakiwa kuwa daraja kati ya viongozi na watumishi wa uma


MOSHI-KILIMANJARO.

Serikali mkoani Kilimanjaro, imewataka Waandishi Waendesha Ofisi (TAPSEA) kwenye ofisi mbalimbali mkoani humo, kuhakikisha kwamba wana kuwa daraja la kuunganisha Viongozi na Watumishi wa Umma kwa kuwa wao ndio vioo vya ofisi.

Katibu Tawala Mkoa wa Kilimanjaro Kiseo Yusuph Nzowa, amesema hayo Novemba 9, 2024, wakati akizindua  chama hicho, hafla iliyofanyika katika  ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa mkoa humo.

Nzowa amewataka TAPSEA hao, kutumia nafasi zao kama njia mojawapo ya kuboresha utendaji kati ya viongozi na watumishi wa umma kwa kuhakikisha mawasiliano baina yao na serikali yanakuwa  ya wazi na yenye tija, kwa kuwa wao ndio wanakutana na viongozi mara nyingi zaidi kuliko watumishi wengine.

“Waandishi Waendesha Ofisi, wanapokuwa makini katika utendaji kazi wao, watasaidia  sana kuwa daraja kubwa na kiungo muhimu kwa viongozi na watumishi wa umma, kwani kwa kufanya hivyo watafanikisha kuleta utulivu, amani, katika ofisi.”amesema Nzowa.

Aidha amesema bila kuwa Waandishi Waendeshaji Ofisi katika taasisi yoyote ile, taasisi hiyo lazima itapwaya kutokana na umuhimu wao na kuwapongeza kwa kuanzisha chama hicho ambacho kitakwenda kuwa na manufaa makubwa katika mkoa huo.

Akisoma risala kwa mgeni rasimi  Ofisi Michael Sedekia, amesema lengo la kuwa na umoja huo ni kuweza kutoa huduma kwa uaminifu, bila kujali muonekano wa mgeni au mwananchi na hivyo  kuunga  mkono juhudi za Rais  Samia Suluhu Hassan katika juhudi zake za kuhakikisha kwamba kila mtanzania anapata huduma inayostahili na kwa wakati.

Aidha amesema TAPSEA mkoa wa Kilimanjaro ina jumla ya Wanachama 145 ambao wametoka katika Ofisi za Serikali na Taasisi mbalimbali za umma na binafsi, huku akiwahamasisha  Waandishi Waendesha Ofisi wengine ambao hawajajiunga na chama hicho kujiunga.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TAPSEA mkoa wa Kilimanjaro Laura Kessy, amesema malengo ya kuanzisha muunganiko huo wa Waandishi waendesha ofisi mkoa wa Kilimanjaro utasaidia kuwa karibu na kuweza kupambana na changamoto zinazowakabili katika maeneo yao ya kazi.

Chama cha waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) kilianzishwa mwaka 2008, ili kuandaa, kudumisha, kutekeleza, kulinda haki, kuwasilisha na kusimamia shughuli zote zinazo husika na waandishi waendesha ofisi mTanzania Bara na Visiwani.

















Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.