Hekta 470 za misitu zaathiriwa na moto

SAME-KILIMANJARO.

Takribani hekta 470 za hifadhi zilizoko katika Kanda ya Kaskazini inayojumuisha mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara, zimeathiriwa na moto katika msimu huu wa kiangazi,  kati ya hizo  hekta 132 zipo Wilaya ya Same yakiwemo baadhi ya maeneo ya hifadhi ya Msitu wa asili Chome (Shengena).

Kaimu Kamanda wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Kaskazini Agustine  Mathias, ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya ufuatiliaji moto katika hifadhi za misitu, yanayolenga kuimariusha utayari wa TFS katika kudhibiti matukio ya moto kwenye Hifadhi za Mazingira Asilia, Hifadhi za Misitu na Misitu ya Kupandwa.

Amesema miongoni mwao sababu za matukio ya moto ni pamoja na kuwepo kwa imani potofu kwamba  baadhi ya watu ambao wanashindana kuchoma moto na yule ambaye moto wake utaenda mbali anaonekana ataishi muda mrefu kuliko wenzake.

Sababu nyingine aliyoitaja ni kuweko kwa shughuli za kijamii, ikiwemo uandaaji wa mashamba, uvunaji holela wa asali, uchomaji mkaa na uwindaji wa wanyama pori nazo pia ni sababu zinachangia kuweko kwa majango ya moto.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Same Kasilida Mgeni, alionya wananchi kuacha mara moja tabia ya kueneza imani hizo potofu kwa jamii, huku akisisitiza kwamba Serikali haitasita kuchukua hatua kali kwa mtu yeyote atakayebainika kuendekeza vitendo hivyo kwani vinasababisha uharibifu wa mazingira.

“Haya mafunzo yamekuja wakati muafaka nimekuwa nikitembea katika maeneo mbalimbali ya Wilaya yangu ya Same, kati ya jambo ambalo limekuwa likichefua sana ni kuona namna wananchi wakichoma moto ovyo jambo ambalo linaharibu mazingira yetu ikiwemo maeneo yetu haya ya hifadhi.” Amesema DC Kasilida.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo Mkuu huyo wa Wilaya alisisitiza  Serikali kuendelea kuchukua hatua za kukabiliana na watu wanaoharibu mazingira kwa kuchoma moto, ambapo pia ameomba jitihada za pamoja kati ya Serikali ya Wilaya na taasisi za uhifadhi zinahitajika ili kuhakikisha wahusika wote watakaobainika kuharibu mazingira wanachukuliwa hatua ili misitu hiyo iendelee kubaki salama.

Katika hatua nyingine mkuu huyo wa Wilaya alielekeza kwa TFS pindi kunapotokea matukio ya moto ni vema wakashirikiana na vyombo vya usalama, likiwemo Jeshi la Zimamoto na Uokoaji  ili kuongeza nguvu katika kuokoa sehemu ya mazingira dhidi ya majanga hayo.



Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.