Masanduku ya Posta bado yana umuhimu wake

Meneja wa Shirika la Posta Mkoa wa Kilimanjaro Bw. Abubakar Athumani, akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusiana na Maadhimishi ya Siku ya Posta Duniani ambayo hufanyika Oktoba 9, ya kila mwaka.

MOSHI-KILIMANJARO.

Meneja wa Shirika la Posta mkoani Kilimanjaro Abubakar Athuman, alisema masanduku ya posta (SLP) bado yana umuhimu haswa ikitiliwa maanani ya kuwa Tanzania imeingia kwenye huduma zinazohusiana na anwani za makazi.

Athuman amesema hayo Oktoba 9,2024 mjini Moshi, mkoani humo, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Posta Duniani kwa Mkoa wa Kilimanjaro, ambapo amesema ni vyema kila mtu, taasisi na hata familia kuwa na anwani zao za masanduku ya posta.

Amesema pamoja na maendeleo ya kiteknolojia ya kisasa bado masanduku ya posta yana umuhimu wake maana hata ukitaka kusajili biashara yako moja wapo ya kigezo kinachohitajika ni anwani ya sanduku la posta.

Aidha amesema kuwa kuanzishwa kwa anawani za makazi kumerahisisha huduma za posta kutokana na ukweli kuwa watu wengi kwa sasa wanapokea mizigo yao majumbani au maofisini mwao moja kwa moja bila kuifika posta.

Amesema huduma ya anwani ya makazi iliyoanzishwa na serikali hivi karibuni, kampuni ya posta wanaitumia kama nyenzo muhimu ya kuwaunganisha na wateja wao.

Kwa upande wake msimamizi wa kitengo cha barua Mkoa wa Kilimanjaro Veronica Magoto, amesema ni muhimu kila mtu na hata taasisi kuwa na sanduku la posta kutokana na kuwa taarifa nyingi zinazotoka serikalini zinahitaji huduma zinazohitaji masanduku ya posta wakati wa mawasiliano.

Naye Afisa Postamasta mkoa wa Kilimanjaro Charles Stephen, ametoa rai kwa Watanzania kujiunga na huduma za duka la kimtandao ili waweze kujulikana na kukuza biashara zao.

Kauli mbiu ya mwaka huu ni miaka 150 ya kuwezesha mawasiliano katika kuboresha maisha ya watu duniani.











 

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.