KIBABOT-SACCOS wapokea gawio la Sh ml 2.2

  MOSHI-KILIMANJARO.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) CPA Habibu Suluo, amekabidhi hundi ya Sh milioni 2.3 kwa Chama cha Ushirika na Mikopo cha Bajaj na Bodaboda mkoani Kilimanjaro (KIBABOT-SACCOS) ikiwa ni gawio la asilimia 20 ya makusanyo ya Sh milioni 12 baada ya kutoa leseni 556.

Aidha Suluo ameipongeza Serikali mkoani Kilimanjaro kwa kuboresha mazingira ya biashara mkoani humo ambayo yamesaidia kila mmoja kuchangia Uchumi wa taifa.

Suluo aliyasema hayo Septemba 3, 2024 wakati wa hafla ya kukabidhi cheti cha Uwakala wa kutoa leseni za LATRA kwa Chama cha Ushirika na Mikopo cha Bajaj na Bodaboda mkoani Kilimanjaro (KIBABOT-SACCOS) hafla iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya mkuu wa mkoa huo.

Mkurugenzi huyo amesema katika kipindi cha kuanzia Mei 2024 hadi Agosti 31 mwaka huu chama hicho kimetoa leseni 556 na kukusanya zaidi ya Sh milioni 12, hivyo LATRA imewaongezea jukumu la kutoa leseni kwa magari ya kukodisha zikiwemo Taix.

“Kwa kipindi cha kuanzia mwezi Mei hadi Agosti 31 mwaka huu, wenzetu wa KIBABOT-SACCOS wametoa leseni 556, katika leseni hizi wameweza kukusanya jumla ya Sh milioni 12,236, 000 na hivyo kuweza kupata gawio la Sh milioni 2,446,400.” Amesema CPA Suluo.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Katibu Tawala wa Mkoa Kiseo Yusuf Nzowa, amesema mkoa huo utaendelea kutoa ushirikiano kwa vijana hao ili kuendelea kukuza Uchumi wao huku akiwasifu kwa kuwa mkoa wa kwanza kuja na ushirika wa aina hiyo nchini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya chama hicho cha Ushirika Amani Bendera, ameipongeza serikali kwa kuwaunga mkono vijana akiahidi kuwa watafanya kazi kwa bidii na kuwa mfano kwa vijana wote nchini.






 

 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.