Halmashauri ya Hai, yapongezwa kujenga Kituo cha Afya kwa Mapato ya ndani

HAI-KILIMANJARO.

Wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Chama cha Mapindizi (CCM) Mkoa wa Kilimajaro, wameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Hai kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025, ambapo imeweza kutenga fedha zinazotokana na mapato yake ya ndani na kujenga Kituo cha Afya Masama Kati.

Hayo yamejiri Septemba 24, 2024, wakati wa ziara ya Kamati ya Siasa mkoani humo, ilipotembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa  Kituo cha Afya Masama Kati, unaotekelezwa kwa mapato ya ndani ya halmashauri hiyo kwa gharama ya SH milioni 209.

Akizungumza mara baada ya kukagua ujenzi wa kituo hicho, Katibu wa CCM mkoa wa Kilimanjaro Mercy Mollel, ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kuwa kinara wa ukusanyaji wa mapato ya ndani  fedha ambazo zimewezesha kujenga kituo hicho cha afya.

“Nikupongeze Mwenyekiti wa Halmashauri ya Hai, Mkurugenzi mtendaji na Wataalamu kwa kusimamia vizuri ukusanyaji wa mapato ya ndani, fedha ambazo zimewezesha kujenga kituo hiki cha afya kupitia mapato yenu ya ndani,”amesema Mollel.

Aidha amesema Serikali ya Awamu ya Sita imeamua kuwasogezea karibu wananchi wake huduma za afya karibu na maeneo ya wananchi.

Akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa Kituo kipya cha afya Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai Dkt.  Itikija Msuya, amesema hadi kukamilika kwa mradi huo utagharimu kiasi cha Sh milioni 209 ambapo hadi sasa  zaidi ya Sh milioni 125 zimekwisha kutumika.

Awali Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai, Edmund Rutaraka, amesema mapato ya ndani, yamezidi kuongezeka kutoka Sh bilioni 4.2 mwaka 2022/2023 hadi kufikia Sh Bilioni 4.5 mwaka 2023/2024.

Diwani wa Kata ya Masama Kati Kandata Kimaro, amesema akina mama wajawazito, walikuwa wakijifungulia njiani kutokana na kukosa huduma za matibabu karibu na eneo hilo.

Katibu Tawala Mkoa wa Kilimanjaro Yusuf Nzowa, amewataka wananchi na watendaji, kuhakikisha kwamba wanailinda na kutunza miundombinu yote inayotekelezwa na Serikali wilayani humo.

“Litakuwa ni jambo la kusikitishasana kama tutasikia miundombinu hii inahujumiwa, tuhakikishe tunailinda kwani serikali imewekeza fedha nyingi na tuipe thamani inayostahili” amesema Nzowa.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Hai Lazaro Twange amesema, melekezo yaliyotolewa na Wajumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa, wameyapokea na kwamba watayafanyia kazi kwa wakati, ikiwemo la kufunguliwa kwa barabara yenye urefu wa kilomita 1.6 ili iweze kupitika kwa muda wote kufika katika kituo hicho cha afya.

Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na makazi ya Mwaka 2022 Kata ya Masma Kati ina jumla ya Wananchi 12,000, hivyo kukamilika kwa mradi huo utakwenda kutatua changamoto ya upatikanaji wa huduma za afya ngazi ya kiytuo cha afya kwenye kata hiyo.
















 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.