Umoja wa Machifu Mkoa wa Kilimanjaro na Baraza la Wazee la Ushauri la Kiserikali mkoani humo, wamempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC).
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Machifu mkoa wa Kilimanjaro Frank Marealle, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Moshi, muda mfupi mara baada ya kumalizika kwa kikao maalum cha Baraza la Wazee la Ushauri la Kiserikali.
Amesema kitendo cha Rais Samia Suluhu Hassan kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa SADC, na kufanikiwa kukiongoza kikao hicho cha Kamati ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), alifanikisha kutatua mgogoro wa kisiasa na kiusalama uliokuwepo katika Ufalme wa Lesotho.
“Kwa niaba ya Machifu wa mkoa wa Kilimanjro na Baraza la Wazee la Ushauri la Kiserikali, tunampongeza Rais Samia kuchaguliwa kuwa mwanamke wa kwanza kuongoza nchi za Southern African Development Community (SADC) tunamuombea kwa Mungu ampe maisha marefu ili aweze kuwatumikia Watanzania na nje ya Tanzania.”amesema.
Chifu wa Siha Godfrey
Kileo, amezipongeza nchi zote za Afrika kwa
kumchagua kushika wadhifa huo kwani wametambua kwamba anaweza kusimamia shughuli
za siasa, ulinzi na usalama, kwetu sisi Tanzania wametupa heshima kubwa.
Awali akizungumza Mwenyekiti
wa Baraza la wazee Mkoa wa Kilimanjaro Eliamini Mkongo, amesema Rais Samia
amefanya kazi kubwa ya kuwaletea maendeleo Watanzania katika nyamba mbalimbali
ikiwemo afya, elimu, maji na miundombinu ya barabara.
Naye Katibu wa Baraza la
Wazee Mkoa wa Kilimanjaro Godson Lucas, tunampongeza Rais Samia kwa kuendelea
kushughulikia masuala ya migogoro baina ya wakulima na wafugaji, pamoja na
kuilinda demokrasia na kusimamia masuala ya ulinzi na usalama kwa nchi yetu.
Kwa upande wake Katibu wa
Machifu mkoa wa Kilimanjaro Joseph Mselle, amesema kwa nafasi aliyopewa ya kuwa mwenyekiti wa
SADAC sehemu inayohusika na mambo ya
siasa, ulinzi na usalama, machifu mkoani humo, wameona iko haja ya kumpongeza
na kumtia moyo ili nafasi aliyopewa aweze kuihudumia vizuri.