Mstahiki Meya Injinia Kidumo: Rais Samia ameridhia ujenzi wa soko Mbuyuni

Rais Samia Suluhu Hassan ameridhia ujenzi wa soko la Mbuyuni lilloungua hivi karibuni uendelee, ambapo tayari mamlaka husika ikiwemo TAMISEMI na Wizara ya Fedha zimesha idhinisha fedha kwa ajili ya kuendelea na ujenzi huo.

Hayo yameelezwa na jana Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro Injinia Zuberi Kidumo, wakati akizungumza na wafanyabiashara mbalimbali ikiwa ni sehemu ya kikao cha Mkuu wa Wilaya ya Moshi Zephania Sumaye alichokiitisha kwa ajili ya kusikiliza kero za wananchi.

“Wakati soko lilipoungua tulikuja kwenye soko hili, kuwajulisha ya kuwa litajengwa upya na kukamilika ndani ya miezi miwili; Baraza la Madiwani tulikaa tukakubaliana ya kuwa kila Kata isitishe mradi mmoja ili fedha za mradi huo zitumike kujenga soko ili wafanyabiashara wasikose mahali pa kufanyia kazi”, alisema Injinia Kidumo.

“Sisi kama Baraza tulishakamilisha taratibu zote lakini kwa vile taratibu zingine zinatutaka kuomba kibali TAMISEMI na kile cha kutoka Wizara ya Fedha ili kuidhinishiwa mabadiliko ya matumizi ya fedha za miradi na ndicho kilichochelewesha kuanza ujenzi wa soko”, alisema.

Aliongeza, “Niwajulishe ya kuwa Rais Samia Suluhu Hassan, ameingilia kati swala hilo na leo ametoa idhini mabadiliko ya matumizi ya fehda hizo kama tulivyoomba na ujenzi unatarajiwa kuanza ndani ya wiki mbili zijazo”, alisema.

Katika hatua nyingine, Meya Kidumo amewapongeza Wanawake kwa kuwa mstari wa mbele katika kurudisha kwa wakati fedha walizokopa ikiwa ni sehemu ya mikopo inayotolewa na halmashauri ya Manispaa ya Moshi.

Aidha ametoa rai kwa maafisa wasafirishaji wa bajaj na bodaboda kujiunga na SACCOS ili kupata huduma ya mikopo nafuu ili waondokane na adha ya kupata mikopo ambayo inakuwa ni vigumu kuirejesha na hivyo kupelekea wao kunyang’anywa zana zao za kazi.

Akijibu maswali kutoka kwa Wafanyabiashara hao, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi Mwajuma Nasombe, amesema tayari halmashauri hiyo imetenga jumla ya snhilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya mikopo ya wanawake, watu wenye ulemavu na vijana.

“Kama mnavyojua mikopo hii ilisitishwa kwa muda; utaratibu wa kutoa mikopo hiyo utakaporudishwa, jitokezeni kwa wingi kuja kukopa maana tayari sisi kama halmashauri tushatenga fedha kwa ajili hiyo”, alisema.

Akijibu changamoto iliyowasilishwa na wafanyabiashara wa soko la mitumba la Meimoria, kuhusu changamoto ya miundombinu isiyo rafiki kwenye eneo la soko hilo hususani wakati wa mvua, Nasombe ameahidi kuwa uongozi wa hamashauri hiyo utaweka moram ili kurudihsia hali nzuri sokoni hapo.


 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.