Jinsi Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia ilivyoibua ukatili aliofanyiwa mtoto wa miaka 5 na Bibi yake

Jinsi Kampeni ya msaada wa Kisheria ya Mama Samia ilivyoibua ukatili aliofanyiwa mtoto wa miaka 5 na Bibi yake

Unyama huo umepelekea mtoto huyo kukatwa mguu.

KISANGARA-MWANGA

Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (MSLAC), imeibua makubwa mkoani Kilimanjaro baada ya kubainika kuna mtoto ambaye amepata ukilema baada ya kufanyiwa ukatili na Bibi yake.

Akizungumzia kisa hicho jana, wakati akitoa elimu kwa wanafunzi wa shule ya sekondari ya Kisangara iliyoko wilaya ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro, Afisa Ustawi wa Jamii Ofisi ya Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya Mwanga Alexs Kameo, alisema mtoto huyo alipata kilema hicho baada ya kupigwa na Bibi yake huyo.

“Mtoto huyo wa miaka mitano alipigwa na Bibi yake ikiwa ni adhabu kwa kile kilichodaiwa ya kuwa alifanya kosa jambo lilipelekea kupata jeraha kubwa juu ya paja la goti”, alisema.

“Hata hivyo Bibi yake huyo alisita kumpeleka hospitali kutibiwa jeraha hilo kwa kuhofia kuwa ikigundulika mtoto huyo amelipata jereha kwa kumwadhibu atachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufungwa jela”, alisema.

Kameo, aliendelea kusema kutokana na hofu hiyo, Bibi huyo aliamua kumfungia mtoto huyo ndani kwa muda mrefu hadi kidonda alichopata mtoto huyo kilioza na kuanza kutoa harufu.

“Kila Bibi alipokuwa akiulizwa na majirani kuhusiana na mtoto huyo yuko wapi, alikuwa akisema amesafiri kwenda kwa ndugu wengine; hata hivyo siku moja wageni waliofika nyumbani kwa Bibi huyo wakasikia harufu kali na kuhoji inatokea wapi na ndipo baada ya kufanywa uchunguzi wa kina ikagundulika mtoto huyo alikuwa amefungiwa ndani”, alisema.

Wageni hao waliamua kwenda kutoa taarifa kwa Mwenyekiti wa kitongoji na ndipo alipokuja na kufungua mlango wa chumba alichokuwa amefungiwa huyo mtoto kna kukutwa akiwa humo ndani akiugulia.

“Mtoto huyo alipelekwa hospitali ya KCMC, lakini ikasemekana mguu wa mtoto huyo tayari umekwisha kuoza na hivyo ikabidi ukatwe”, alisema.

Hata hivyo kila mtoto huyo alipokuwa akiulizwa ni nini kilichompata alikuwa akisema ya kuwa ameumizwa na mtoto mwenzake wakati wakicheza.

“Baada ya kupata huduma KCMC mtoto huyo alipelekwa kwenye kituo cha malezi ya watoto na pale  walifika Wanasaikolojia na kuzungumza na mtoto huyo ili kutaka kupata ukweli wa kile kilichomsababishia mguu wake kukatwa.

Katika simulizi yake hiyo, Kameo alisema mtoto huyo baada ya kuhojiwa kwa kina na Wanasaikolojia akakiri ya kuwa Bibi yake ndiye alimuadhibu na alipopata jereha hilo alimwambia akisema kuwa alimpiga tamuua ndipo akaogopa kusema”, alisema.

“Tumeona umuhimu wa kwenda kwenye shule hiyo ili kutoa elimu kuhusiana na Msaada wa Kisheria, lakini pia tumewafundisha elimu kuhusiana na sheria ya mtoto ili waweze kujua kwamba wana wajibu gani na haki gani kulingana na miongozo ya kisheria,”alisema.

Alisema aliamua kuwaelezea kisa hicho ili kuwajengea uwezo kwamba wanao ujasiri wanaweza kujikwamua kutoka kwenye mnyororo wa kufungwa, kushindwa kutoa taarifa, au kwa kuhisi kwamba wakitoa taarifa wazazi wao watakuwa na changamoto za kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Mtoto huyu ni yatima baada ya kupoteza wazazi wake wote wawili na kwa mujibu wake yeye mweyenyewe anampenda Bibi yake na anamtegemea hivyo akaogopa kusema yaliyompata kwa kuhofia bibi yake atafungwa na atabaki na nani”, alisema.

Alisema baada ya shauri hilo kupelekwa polisi na hatimae kufikishwa mahakamani lakini likaondolewa mahakamani hapo baada ya kukosa ushahidi.

“Huu ni mfano mmoja tu wa mambo mengi ambayo watoto wengi na hata watu wazima wanafanyiwa ukatili wa aina mbalimbali lakini wanashindwa kuripoti vitendo wanavyofanyiwa kwa ajili ya vitisho wanavyopata kutoka kwa waliowafanyia vitendo vya ukatili”, alisema.

Kwa upande wake Afisa Wahudumu Msaada wa Kisheria Innocent Muro, alisema Rais Samia baada ya kuona changamoto hizo aliona kuna haja ya kuwa na kitengo cha Msaada wa Kisheria kwa wananchi ambao wanashindwa kukidhi gharama za kuendeshea mashtaka yao pindi yanapokuwa katika mahakama.

“Baadhi ya watu ambao wanakumbwa na changamoto za Huduma ya Msaada wa Kisheria ni watu wenye vipato vya chini, wako watu wenye uwezo wa kipato cha kifedha wanatumia kama shehemu ya kuwakandamiza watu wenye uchumi mdogo kuwanyima haki zao.”alisema.

Pia Muro alielezea  Kampeni hiyo yenye maudhui ya kusaidia wananchi ina mambo 10 na itapita kila eneo la Tanzania Bara na Visiwani, ambapo kwa Wilaya ya Mwanga Kampeni hiyo wamevifikia vijiji vitatu vya Mangara, Mbambua na Kisangara vilivyoko Kata ya Lembeni, pamoja na shule ya sekondari Kisangara na shule ya msingi Kisangara.







Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.